TOTO'S CORNER
Saturday, 31 January 2015
Wednesday, 28 January 2015
AN ARTICLE ABOUT ADVANTAGE AND DISADVANTAGE OF GLOBALZATION FOR YOUTH
Suala la utandawazi si
geni miongoni mwa masikio ya watu ni kama imekuwa sehemu ya maisha yetu ya kila
siku kwa wale ambao wapo ndani ya utandawazi na wale wenzangu na mie ambao wameishia kuwa ni
mashabiki na mashuhuda wa Utandawazi. Rasmi utandawazi ulianzia miaka ya
Themanini lakini ukaanza kushika kasi
miaka ya Elfu mbili. Ni wazi kuwa katika maisha ya sasa utandawazi umekuwa na
mchango mkubwa sana katika mambo mengi sana ikiwemo malezi ya Watoto na Vijana kwa ujumla. Sote ni mashahidi
katika hili. Kwa mfano ukikaa na watu wazima ambao walikuwa katika miaka ya
Hamsini hadi mwanzoni mwa themanini ni wazi watakueleza tofauti za kimalezi
miongoni mwa vijana na watoto. Ni wazi kwamba watoto na vijana wa sasa wamekuwa
na uelewa mkubwa wa mambo mengi ya maisha katika Nyanja mbalimbali. Mtoto mdogo
ana uwezo wa kutumia vitu mbalimbali vinavyokuja kwa mkumbo wa utandawazi kama
vile simu,Kompyuta,na vitu vingine vya kisasa bila hata ya kufundishwa hali
ambayo ni tofauti na ilivyokuwa miaka hiyo na ndiyo maana wazee wengi
hupendelea kusema kwamba watoto wa kisasa ni watundu tofauti na hali ilivyokuwa
kipindi kile hili liko wazi.
Tatizo linakuja kwamba pamoja na kwamba vijana na watoto wa miaka ya hivi sasa wamekuwa na uelewa wa haraka lakini kasoro yao ambayo inawatofautisha na vijana wa zamani ni ukosefu wa Maarifa juu ya mambo mengi na pia matumizi mazuri ya huu Utandawazi. Kwa kweli Utandawazi ambao ulitegemewa kuwa kama mkombozi wa kijana hasa wa Kitanzania katika mambo mengi badala yake Utandawazi umekuwa kama chanzo cha kumpotosha kijana wa Kitanzania hasa waliopo Shuleni ambao wamekuwa ni Waathirika wakubwa wa Utandawazi. Sikatai kwamba Utandawazi umekuwa mkombozi mkubwa kwa baadhi ya vijana na wanafunzi ambao wamekuwa na Utajiri wa Maarifa kama walivyokuwa vijana wa miaka ya Sabini ambao wengi wao hawakuwa na uwezo wa kupata Elimu lakini walikuwa na Maarifa ya Maisha katika Nyanja mbalimbali. Kwa kweli kuna vijana ambao wamekuwa wakitumia Utandawazi kwa Upande chanya zaidi hasa wale wasioendekeza starehe na Anasa za maisha ambao wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii kama sehemu ya darasa kwao kwa kutafuta vitabu vitu vingine ambavyo vinawasaidia katika masomo na ndio hawa hawa ambao tunawaona na mafanikio katika maendeleo yao
TWITTER
WATSAPP
INSTAGRAM
Facebook ,Twitter
,Whatsup ,Instagram na mitandao mingine ya kijamii imekuwa ni kijiwe sasa Baada
ya vijiwe vile ambavyo wazazi walikuwa wanavipiga vita. Sasa ni wakati wa
wazazi kuelewa sasa kwamba vijiwe hivyo sasa vimeamia katika mitandao ya
kijamii vikichangiwa na hizi zinazoitwa (Blogs) ambapo imekuwa ni kawaida kwa
vijana ukamkuta yupo hewani masaa yote. Hadi inafika kipindi unaweza kujiuliza
kama kijana huyo ameajiriwa na mtandao husika au ni vipi. Kwa kweli hali ni ya
kutisha hasa kwa wanafunzi wa Sekondari hasa za Serikali. Wazazi wamefanikiwa
kuwazuia mabinti zao kuwa huru kwa asilimia Fulani lakini wamesahau uwepo wa
simu za mikononi kama uwanja mpya wa kudanganyana na pia kwa mafataki kuweza
kupenya katika nyumba zao mpaka kwa mabinti zao kuweza kuwalaghai kupitia simu
za mikononi na mwisho wa siku ijulikane kwamba kwa nafasi kidogo watakayoipata
basi wajue mambo yatakuwa yashaharibika.
Kwa vijana mitandao kama Istagram na Facebook imekuwa kama sehemu ya kujiuza na kunadi biashara ya mwili. Hili lipo wazi kupitia picha za nusu uchi ambazo vijana wengi wa kike wamekuwa wakiziweka katika kurasa zao cha kushangaza zaidi mpaka wanafunzi wa vyuo vikuu wamekuwa ni mashabiki wakubwa wa mchezo huo wa aibu lakini cha kuogofya zaidi ni kwa wanafunzi wa kike wa sekondari kuambukizwa kamchezo hako kabaya na cha kukemea kwa hali yoyote na gharama yoyote ingawa wenyewe huitaji uhuru katika masuala mbalimbali ya maisha lakini yatupasa tujue kwamba huu si uhuru sasa bali ni Udhalilishaji binafsi kwao na kwa familia zao hasa kwa wazazi ambao wamekuwa wakihangaika usiku na mchana kuwasaidia watoto wao waweze kusoma na kuwa na maisha mazuri.
Kwa vijana mitandao kama Istagram na Facebook imekuwa kama sehemu ya kujiuza na kunadi biashara ya mwili. Hili lipo wazi kupitia picha za nusu uchi ambazo vijana wengi wa kike wamekuwa wakiziweka katika kurasa zao cha kushangaza zaidi mpaka wanafunzi wa vyuo vikuu wamekuwa ni mashabiki wakubwa wa mchezo huo wa aibu lakini cha kuogofya zaidi ni kwa wanafunzi wa kike wa sekondari kuambukizwa kamchezo hako kabaya na cha kukemea kwa hali yoyote na gharama yoyote ingawa wenyewe huitaji uhuru katika masuala mbalimbali ya maisha lakini yatupasa tujue kwamba huu si uhuru sasa bali ni Udhalilishaji binafsi kwao na kwa familia zao hasa kwa wazazi ambao wamekuwa wakihangaika usiku na mchana kuwasaidia watoto wao waweze kusoma na kuwa na maisha mazuri.
Wakati haya yote yakiendelea wazazi wamekuwa hawaelewi chochote kinachoendelea kwa vijana wao. Kwa kweli watu wengi wamekuwa wakiwalaumu wazazi kuhusu suala la malezi na Uangalifu wa watoto wao lakini mimi bado lawama zangu zipo kwa vijana wenyewe pamoja na matumizi mabaya ya Utandawazi. Ni vigumu kwa mkulima kujua ni nini kinachoendelea katika mitandao wakati hana hata uelewa wa uwepo wa mitandao hiyo ya kijamii. Ni kichekesho kumuulizia mkulima kutoka Tanga vijijini kuhusu suala la Instagram wakati hata hiyo Facebook yenyewe tu haijui. Wengi wamekuwa ni watumiaji wa Redio na suala la mitandao kwa kweli limewatupa mkono hivyo ni vigumu sana kujua ni nini kinachofanywa na vijana wao ndani ya mitandao ya kijamii kwa hiyo ni makosa sana kuwalaumu kuhusu hilo kwani sababu kubwa ya haya yote ni vijana wenyewe hasa wale wanaopenda kuishi maisha ya kufuata mkumbo.
Kwa kweli suluhisho kubwa ni kutoa Elimu kwa vijana juu ya matumizi mazuri ya mitandao ya kijamii ambayo imekuja kwa mkumbo wa Utandawazi lakini pia kama ambavyo kumekuwa na fuatiliaji mkubwa wa kimaadili katika mambo mengine lakini imefika wakati ambao serikali na vyombo vinavyohusika pia kufuatilia suala la maadili katika mitandao ya kijamii juu ya suala zima la Picha chafu na pia matumizi ya lugha chafu za matusi katika mitandao kwani imekuwa ni fasheni katika mitandao vijana kuweka picha chafu kwa mfano katika Facebook Yule ambaye huweka picha nyingi chafu na zinazoonesha kuwacha wazi sehemu kubwa ya mwili mara nyingi wamekuwa na idadi kubwa ya marafiki na mashabiki wenyewe wanawaita watu maarufu ndani ya facebook kana kwamba wanalipwa. Kwa kweli hali inasikitisha hasa kwa nchi yetu hii ambayo tunasema vijana ndiyo taifa la kesho. Kwa hali hii inavyoenda taifa la kesho litakuwa ni uchafu mtupu ndani ya jamii kama hatutadhibiti hii hali ya kuendekeza utandawazi na kuwapa uhuru vijana katika kufanya mambo mbalimbali. Yangu ni hayo tu kwa leo nawatakia mafanikio katika vita hii dhidi ya matumizi mabaya ya Utandawazi kwa vijana wetu.
Subscribe to:
Posts (Atom)